JIMBO LA MUSOMA NA WATU WAKE

JIOGRAFIA YA JIMBO KATOLIKI LA MUSOMA 
Kabla ya kuundwa kwa Jimbo Jipya la Bunda, Novemba 27, 2010, Jimbo la Musoma lilikuwa na mipaka ya ukubwa sawa na ile ya Mkoa mzima wa Mara – ambao uko Kaskazini mwa Tanzania. Kwa sasa, Jimbo la MUSOMA linapakana na majimbo ya Bunda (lililozaliwa toka Musoma na Mwanza), upande wa kusini Arusha na nchi ya Kenya upande wa mashariki. Sehemu kubwa ya upande wa Mashariki mwa Jimbo zinakutwa mbuga za wanyama za Serengeti ambapo jimbo la Musoma linapakana na majimbo ya Shinyanga na Mbulu. Kwa ukubwa, kwa sasa (tukiondoa Jimbo la Bunda), Jimbo la Musoma linakadiriwa kuwa na ukubwa wa Kilomita za Mraba zipatazo 24,019.
WAKAZI WA MKOA WA MARA
Hadi kufikia Mwaka 2004, idadi ya wakazi wa Mkoa wa Mara ilikuwa ni takribani watu wapatao 1,400,000 na kati ya hao watu takribani 260,000 wakiwa ni wakazi wa Wilaya ya Bunda. Idadi ya Wakatoliki ilikuwa ni takribani watu 250,000 sawa na asilimia 17.9. Kwa upande wa makabila yanayokutwa Mkoa wa Mara, yako mengi. Baadhi ya hayo ni yafuatayo: Waluo, Wajita, Waruri, Wazanaki, Wakurya, Wakabwa, Wakiroba, Wasimbiti, Wangoreme, Wakwaya,Waikoma, Wanata, Waisenye, Waikizu na Walieri.
MAISHA YA IMANI KABLA YA UJIO WA WAMISIONARI
Kama tunavyojifunza kutoka katika Katekisimu ya Kanisa Katoliki kuwa, tamaa na kiu ya Mungu imeandikwa na Mungu mwenyewe ndani ya kila mwanadamu (Katekisimu ya Kanisa Katoliki. n. 27 - 28) hali kadhalika, kabla ya Ujio wa Wamisionari, wenyeji wa Mkoa wa Mara nao walionesha kiu yao kwa namna mbalimbali.

Wenyeji wa Mkoa wa Mara, tangu zamani walikuwa na Imani zao za jadi, kuheshimu (au kuabudu) jua na viumbe vingine kama vile miti mikubwa, miamba, mapango, mito mikubwa, majoka makubwa, na viumbe vingine kama hivyo. Hali kadhalika wapo walioamini katika uchawi na ushirikina, kupiga ramli, matambiko, mazindiko, mizimu, na mambo mengi tu ya giza. Walitafuta majibu ya maswali yao magumu kutoka katika nguvu hizi.

Hivyo, haikuwa rahisi kwao kubadilika na kuupokea ukristo mara moja na kwa urahisi, na hata baadhi ya wale waliopokea Imani ya Kikristo walijikuta wanashindwa kubandukana na imani yao ya jadi, na kuishia kuchanganya yote mawili, Ukristo na Imani za jadi (syncretism), hali ambayo bado ipo hadi leo hii katika baadhi ya maeneo.

Sambamba na imani za namna hiyo (kama zilivyotajwa hapo juu), bado pia walikuwa na mila na desturi zingine ambazo ni kinyume cha Ukristo, kama vile, kuoa wake wengi, kutupa watoto waliozaliwa mapacha, nyumba ntobhu (katika jamii za Wakurya), kurithi wajane (katika jamii za waluo).

Hii ndiyo ilikuwa picha ya jumla katika jamii za wenyeji wa Mkoa wa Mara kuhusiana na suala zima la imani zao kabla ya ujio wa wamisionari.


No comments

Kamati zapewa mafunzo ya kupambana na ukatili

KAMATI za kupambana na masuala ya ukatili wa kijinsia katika halmashauri ya wilaya ya Rorya zimepewa mafunzo ya kupambana na masuala ya ...

Powered by Blogger.